Ticker

6/recent/ticker-posts

Faida Za Nanasi Mwilini mwako,Soma hapa kufahamu



Nanasi ni tunda la kitropiki ambalo huchukua miaka mitatu kukomaa. Nanasi ni tamu, huongeza vitamini na virutubisho mbalimbali kwa afya ya mlaji. Pia hupambana na magonjwa.

Nanasi lina faida mbalimbali za afya, ikiwa ni pamoja na kuboresha usagaji wa chakula, kuondoa hatari ya saratani, na kuondoa maumivu.

Hata hivyo, wale walio na mzio wanapaswa kuepuka matunda haya na wale wanaotumia dawa za kupunguza damu wanapaswa kuwa waangalifu.

Kupambana na magonjwa

Tunda hili lina utajiri mkubwa wa vitamini C na magnishiamu. Vitamini C ni muhimu katika kusaidia kinga ya mwili.

Magnishiamu husaidia kupambana na seli zinazoweza kuleta madhara katika mwili, husaidia kuzuia uvimbe ambao unaweza kusababisha saratani na magonjwa mengine sugu.

Nanasi ni chanzo muhimu cha kupambana na magonjwa. Kutumia nanasi mara kwa mara kunaweza kukupunguzia hatari ya kupata ugonjwa wa moyo na kisukari.

Usagaji wa chakula

Tunda hili lina enzaimu wa kusaidia usagaji chakula waitwao bromelain, ambao husaidia kurahisisha usagaji wa chakula.

Bromelain huvunja molekuli za protini, ikimaanisha utumbo wako mdogo unaweza kuzifyonza kwa urahisi zaidi.

Hilo ni muhimu sana kwa watu walio na upungufu wa maji ya kongosho, hali inayoifanya kongosho kutotengeneza vimeng’enya vya kutosha vya kusaga chakula.

Kwa kuwa lina nyuzinyuzi nyingi, pia husaidia mfumo wa usagaji chakula na kuboresha afya ya vijidudu vyenye faida ambavyo hukaa kwenye utumbo wako.

Uponyaji baada ya kuumia

Tafiti kadhaa zinaonyesha kuwa bromelain ambayo pia inapatikana katika nanasi, husaidia kupunguza uvimbe na michubuko baada ya jeraha au upasuaji.

Nanasi linaweza kuwa muhimu ikiwa utakula kabla ya ung’oaji wa jino, husaidia kupunguza maumivu na kutoa ahueni kama vile dawa ya kuzuia maambukizi.

Utafiti wa taasisi ya Vitro (uliofanywa katika maabara), pia umeonyesha bromelain husaidia katika uponyaji wa jeraha.

Kupunguza maumivu ya viungo

Tatizo la maumivu ya viungo, ni ugonjwa unaohusisha viungo kuvimba, kuwa vyekundu na kuleta maumivu. Ugonjwa huu ni matokeo ya mfumo wa kinga kushambulia tishu zenye afya kimakosa.

Tafiti nyingi, zilizoanzia miaka ya 1960, zimeonyesha jinsi bromelaini inavyoweza kuwa muhimu katika kutuliza maumivu yanayohusiana na viungo.

Maumivu ya viungo huathiri zaidi ya watu wazima milioni 54 huko Marekani. Kuna aina nyingi za ugonjwa wa maumivu ya viungo, lakini mengi ya magonjwa hayo huhusisha kuvimba kwa viungo.

Virutubisho vya bromelaini, husaidia kuondoa maumivu katika sehemu ya chini ya mgongo kama sawa na matibabu ya maumivu.

Kusaidia kinga ya mwili

Utafiti wa wiki tisa wa watoto wa shule ambao walikula kiasi cha wastani cha mananasi kila siku, walikuwa na hatari ndogo sana ya kuambukizwa virusi au bakteria kuliko wale ambao hawakula.

Mbali na hayo, wale waliokula kiasi kikubwa walipata mara nne ya idadi ya seli nyeupe za kinga za kupambana na maambukizi.

Nanasi pia kusaidia kurekebisha mfumo wa kinga, na linaweza kuwa bora kwa wale walio na kinga dhaifu za mwili.

Kusaidia mfumo wa moyo

Kwa mara nyingine tena, ni bromelain ambayo inaonekana kuwa na umuhimu kwa moyo na mfumo wa mzunguko wa damu, kwa kuzuia au kupunguza ukali wa mshtuko wa moyo.

Uchunguzi kwa wanyama unaonyesha bromelain pia huzuia shinikizo la damu, kuganda kwa damu kwa kuzuia utengenezwaji wa protini inayoitwa fibrin ambayo inahusika katika kuganda kwa damu.

Kupunguza hatari ya pumu

Juisi ya nanasi pia inaweza kuwa na ufanisi katika kupunguza dalili zinazohusiana na pumu. Katika utafiti wa wanyama, watafiti waligundua kuwa bromelain zinaweza kuwa na faida kwa watu wanaoishi na pumu.

Zaidi ya hayo, nanasi lina vitamini C, ambavyo hulainisha mirija ya mapafu. Na katika matukio ya mashambulizi ya pumu kutokana na baridi, vitamini C vilikuwa ya manufaa

Nanasi ni salama kwa kila mtu?

Kama huna mzio na nanasi, kwa ujumla inatambulika kuwa nanasi ni salama kwa watu wengi na ni sehemu ya lishe bora.

Hata hivyo, kula au kunywa kiasi kikubwa kunaweza kusababisha shida ya usagaji chakula. Jambo jingine ni kujiepusha kula nanasi ambalo halijaiva kwa sababu, linaweza kusababisha kuhara na kuwasha koo.

Zaidi ya hayo, ikiwa unakabiliwa la asidi ya reflux, nanasi linaweza kuongeza dalili zako. Asidi hiyo inaweza kusababisha kiungulia.

Wale wanaotumia dawa za kupunguza damu wanapaswa kukumbuka kwamba bromelaini iliyo katika nanasi inaweza kuathiri uwezo wa damu kuganda na inapoliwa kwa wingi, na kwa kushirikiana na dawa za kupunguza damu, inaweza kuongeza hatari ya kutokwa na damu.

Licha ya faida zake, ni muhimu kukumbuka kuwa juisi ya mananasi ina nyuzinyuzi kidogo lakini ina sukari nyingi sana.

Hii inamaanisha haitakuwa na uwezo wa kukujaza tumbo lako kama kula nanasi la kawaida la kiwango hicho hicho, lakini inaweza kusababisha uzito kwa baadhi ya watu.

Via:Bbc





Post a Comment

0 Comments