Ticker

6/recent/ticker-posts

COVID-19: Maambukizi yaongezeka kwa asilimia 52 katika mwezi mmoja, yasema WHO



COVID-19: Maambukizi yaongezeka kwa asilimia 52 katika mwezi mmoja, yasema WHO.

Shirika la Afya Duniani, WHO, jana limethibitisha idadi ya wagonjwa wa COVID-19 duniani kote inaongezeka kwa kasi na kwamba “tutarajie idadi kubwa zaidi ya wagonjwa katika miezi ijayo ya msimu wa baridi kali kwenye maeneo ya kaskazini mwa dunia.”

Takwimu za hivi karibuni kutoka WHO zikijikita katika wiki nne za kuanzia mwezi Novemba hadi Desemba 17 mwaka 2023 zinaonesha ongezeko la asilimia 52 ya idadi ya wagonjwa ikilinganishwa na siku 28 zilizotangulia.

Msemaji wa WHO Christian Lindmeier, amewajulisha waandishi wa habari mjini Geneva, Uswisi hii jana kuwa ongezeko hilo ni sawa na wagonjwa wapya 850,000, lakini takwimu kamili zinaweza kuwa za juu.

“Unafahamu kuwa duniani kote na umeshuhudia hata wengi wenu kwenye nchi zetu kwamba utoaji wa taarifa umepungua, vituo vya ufuatiliaji navyo vivyo hivyo, kwingine vimevunjwa kabisa au vimefungwa… kwa hiyo hii bila shaka inatupeleka kwenye kukosa picha halisi na tunatarajia kwa bahati mbaya idadi kubwa zaidi ya wagonjwa kuliko tulivyoripoti,” amesema Bwana Lindmeir.

Maambukizi mengi yamesababishwa na aina na mnyumbuliko mpya wa COVID uitwao JN.1 ambao kwa sasa unachunguzwa kwa kina na WHO kama mnyumbuliko unaopaswa kufuatiliwa kwa karibu.

Kwa mara ya kwanza aina hiyo  JN.1 ilibainika Marekani kabla ya kusambaa kwenye maeneo mengine kadhaa ya nchi.

Inatokana na mnyumbuliko wa COVID uitwao Omicron ambao ulihusishwa na ongezeko kubwa la maambukizi ya COVID-19 mwaka 2022.



Post a Comment

0 Comments