Ticker

6/recent/ticker-posts

Awekewa kifaa cha kuusaidia moyo kufanya kazi vizuri “Pacemaker”



Mgonjwa awekewa kifaa cha kuusaidia moyo kufanya kazi vizuri “Pacemaker”

Mgonjwa aliyefanyiwa uchunguzi katika kambi maalumu ya matibabu ya moyo iliyofanyika mkoani Kagera wiki iliyopita awekewa kifaa cha kuusaidia moyo kufanya kazi vizuri “Pacemaker”.

Mgonjwa huyo alikuwa na matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo hivyo mapigo yake ya moyo kuwa chini ya 50 na kupata changamoto za kizunguzungu na wakati mwingine kupoteza fahamu.
Akizungumza na mwandishi wa habari hii daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na mfumo wa umeme wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Yona Gandye alisema baada ya mgonjwa huyo kufanyiwa uchunguzi katika kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan outreach services iliyofanyika mkoani Kagera na kugundulika kuwa na tatizo la mfumo wa umeme wa moyo alipewa rufaa kufika JKCI kwaajili ya matibabu zaidi.

Dkt. Gandye alisema mgonjwa huyo amechuka hatua za haraka kufika ambapo amefanyiwa uchunguzi zaidi na baadaye kufanyiwa upasuaji mdogo wa moyo kwa kutumia mtambo wa cathlab kuwekewa kifaa cha kuusaidia moyo kufanya kazi vizuri (Pacemaker).

“Kikawaida mapigo ya moyo yanatakiwa kuanzia 50 hadi 100 kwa dakika moja, mgonjwa huyu mapigo yake yalikuwa chini ya 50 lakini baada ya matibabu mapigo yake yamekuwa yakawaida”, alisema Dkt. Gandye
Dkt. Gandye alisema baada ya kumalizika kwa kambi hiyo ijumaa ya wiki iliyopita hadi sasa wagonjwa watatu kati ya 55 waliopewa rufaa kufika JKCI kwaajili ya matibabu zaidi wamefika na kupatiwa huduma.

Kwa upande wake mgonjwa kutoka Kagera AnaJoyce Laurent alisema hakuwahi kujua kama na tatizo la shinikizo la juu la damu na matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo hadi hapo alipofika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Bukoba (BRRH) wiki moja kabla ya kambi maalumu ya matibabu ya moyo akiwa na tatizo la kichomi.

AnaJoyce alisema baada ya kufanyiwa uchunguzi wataalamu wa afya wa BRRH walimshauri kufika katika kambi maalumu ya matibabu ya moyo iliyokuwa ikiendeshwa na JKCI kuonana na daktari bingwa wa moyo kutokana na mapigo yake ya moyo kuwa chini ya 50.

“Nilifuata ushauri wa madaktari na kuonana na bingwa wa moyo wa JKCI jumatatu iliyopita wakati wa kambi maalumu ya matibabu ya moyo ambaye alinishauri kufika JKCI mapema kufanyiwa upasuaji mdogo wa moyo kuwekewa pacemaker”



Post a Comment

0 Comments