Ebola
Ebola yagunduliwa jimbo jipya nchini Congo,Hofu yaongezeka
Ebola yagunduliwa jimbo jipya nchini Congo,Hofu yaongezeko
Mamlaka za afya katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zimethibitisha kifo cha mtu aliyekuwa ameambukizwa ugonjwa wa Ebola katika jimbo ambalo hapo awali halikuwa limeathirika na mlipuko wa ugonjwa huo.
Kifo hicho kimeibua hofu ya kuenea zaidi kwa maambukizi, kutokana na idadi kubwa ya watu waliokutana na mgonjwa huyo kabla na baada ya kifo chake.
Marehemu anatajwa kuwa dereva wa bodaboda aliyesafiri kutoka jimbo la Haut-Uele, ambako tayari kulikuwa na visa vilivyothibitishwa vya Ebola, kwenda jimbo la Bas-Uele, ambalo hadi wakati huo halikuwa limeripoti mgonjwa yeyote wa Ebola.
Mkuu wa Taasisi ya Kitaifa ya Utafiti wa Tiba ya Biolojia, Jean-Jacques Muyembe, amesema dereva huyo wa bodaboda alifariki katika mji wa Buta, mji mkuu wa jimbo la Bas-Uele, baada ya kutokwa na damu, dalili zinazohusishwa na Ebola.
Vipimo vilivyofanywa baada ya kifo chake vilithibitisha alikuwa tayari ameambukizwa virusi vya Ebola.
Muyembe ameongeza kuwa kabla ya kufariki, marehemu alitembelea vituo kadhaa vya afya.
Aidha, madereva wenzake wa bodaboda walijaribu kuuchukua mwili wake, jambo lililolazimu polisi wa eneo hilo kuingilia kati. Tukio hilo limeongeza hofu kwamba huenda watu kadhaa waliambukizwa virusi vya Ebola.
