Hospital
Candida auris: Fangasi Hatari Anayeenea Katika Mazingira ya Hospitali
Fangasi aina ya Candida auris (C. auris) wanaendelea kuwa tishio linaloongezeka katika maeneo ya huduma za afya, hasa hospitali na vituo vya kulelea wagonjwa. Taarifa za hivi karibuni kutoka Marekani zinaonyesha ongezeko kubwa la visa vya maambukizi mwaka huu.
Kwa mujibu wa takwimu za CDC, kufikia Julai 25, 2026, kulikuwa na visa 3,437 vya kliniki katika majimbo 27 ya Marekani, ikilinganishwa na visa 4,290 vilivyoripotiwa kwa mwaka mzima wa 2025.
Candida auris ni nini?
Candida auris ni aina ya Fangasi (yeast),Tofauti na fangasi wengi wa kawaida, C. auris inaweza kuenea kwa kugusana na mtu aliye nayo au kupitia vifaa na mazingira yaliyochafuliwa.
Changamoto kubwa ni kwamba fangasi huyu anaweza kubaki kwenye mazingira ya hospitali kwa muda mrefu na kuwa sugu kwa baadhi ya bidhaa zinazotumika kusafisha na kuua vijidudu.
Kwa sababu hiyo, hospitali na vituo vya huduma kwa wagonjwa huhitaji kuchukua tahadhari maalumu pale inapobainika kuwa mgonjwa ana C. auris.
Kwa nini Candida auris ni hatari?
Moja ya sababu zinazoufanya C. auris kuwa tishio kubwa ni uwezo wake wa kuwa sugu kwa dawa kadhaa za kuua fangasi.
CDC imewataja kama tishio kwa afya ya umma kwa sababu baadhi ya aina zake zinaweza kuwa sugu kwa makundi yote matatu makuu ya dawa za antifungal zinazotumika kutibu maambukizi ya fangasi.
Hata hivyo, si kila mtu anayepatikana na C. auris huwa mgonjwa.
Mtu anaweza kuwa na fangasi hawa bila dalili zozote
Kuna hali mbili muhimu za kuelewa.
Kwanza ni colonization, ambapo C. auris inaweza kuwepo kwenye ngozi ya mtu bila kusababisha ugonjwa. Mara nyingi mtu huyu hana dalili.
Pili ni maambukizi (infection), ambapo fangasi huingia ndani ya mwili na kusababisha ugonjwa. Hii inaweza kutokea hasa pale mtu anapokuwa na kinga dhaifu au kuna sehemu ya ngozi iliyoharibika inayoweza kuruhusu fangasi kuingia mwilini.
C. auris inaweza kugunduliwa kwa kutumia sampuli inayochukuliwa kwenye maeneo kama kwapa au kinena.
Nani yuko kwenye hatari zaidi?
C. auris huwa tatizo kubwa zaidi kwa watu ambao tayari wana matatizo mengine ya kiafya, hasa wale wanaolazwa hospitalini.
Watu walio katika mazingira ya hatari zaidi wanaweza kujumuisha wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji, wanaopokea chemotherapy, wenye kinga dhaifu au wanaotumia antibiotics kwa muda.
Hii ndiyo sababu C. auris si tishio linalowahusu watu wote kwa kiwango sawa. Mara nyingi huonekana kama changamoto kubwa ndani ya hospitali na vituo vya huduma za muda mrefu.
Dalili za maambukizi ya Candida auris
Mtu ambaye C. auris amekaa kwenye ngozi bila kusababisha maambukizi anaweza asiwe na dalili yoyote.
Lakini fangasi akiingia kwenye mwili na kusababisha maambukizi makubwa, hasa kwenye damu, mgonjwa anaweza kupata dalili kama:
- Homa
- Mapigo ya moyo kwenda kwa kasi
- Shinikizo la damu kushuka
- Dalili za maambukizi makubwa mwilini
- Sepsis katika hali mbaya
Sepsis ni hali hatari inayotokea mwili unapotoa mwitikio mkali dhidi ya maambukizi na inaweza kusababisha kushindwa kwa viungo muhimu vya mwili.
Je, Candida auris inaenea kwa njia gani?
C. auris inaweza kusambaa kupitia mgusano wa moja kwa moja na mtu aliye nayo, au kwa kugusa vitu na vifaa vilivyochafuliwa.
Tatizo kubwa ni uwezo wake wa kubaki kwenye mazingira ya huduma za afya. Kwa hiyo, usafi wa mikono, usafishaji sahihi wa mazingira na kutokushirikisha vifaa vya matibabu kabla havijasafishwa na kutakaswa ni hatua muhimu za kuzuia kuenea kwake.
Hospitali pia zinaweza kufanya uchunguzi wa wagonjwa walio katika hatari ili kubaini kama wamebeba fangasi huyo hata kama hawana dalili.
Kwa nini visa vinaonekana kuongezeka?
Ingawa ongezeko la visa linaweza kuonekana kuwa la kutisha, wataalamu wanaonya kwamba sehemu ya ongezeko hilo inaweza kuhusishwa pia na ongezeko la upimaji.
Vipimo vya uchunguzi vinaweza kubaini watu ambao wamebeba C. auris bila kuwa na maambukizi makubwa. Kwa hiyo, ni muhimu kutofautisha kati ya mtu ambaye amekuwa colonized na mtu ambaye ana maambukizi yanayosababisha ugonjwa.
Hata hivyo, wataalamu bado wanaona C. auris kama tishio muhimu linalohitaji ufuatiliaji na tafiti zaidi.
Nini kifanyike kuzuia kuenea?
Kwa watu waliolazwa hospitalini au wanaoishi katika vituo vya huduma, hatua muhimu ni kuzingatia kanuni za usafi na udhibiti wa maambukizi.
Kunawa mikono vizuri, kuhakikisha vifaa vya matibabu vinasafishwa na kutakaswa kabla ya kutumiwa kwa mtu mwingine, pamoja na kusafisha mazingira ya huduma za afya kwa bidhaa zinazofaa, ni sehemu muhimu ya kuzuia kuenea kwa C. auris.
Iwapo mtu amegundulika kuwa na C. auris, ni muhimu pia wahudumu wa afya kujua hali hiyo ili waweze kuchukua hatua zinazofaa za kuzuia maambukizi kusambaa kwa wagonjwa wengine.
Je, kila mtu anapaswa kuwa na hofu?
Hapana.
Wataalamu wanaeleza kwamba C. auris ni tatizo kubwa zaidi kwa wagonjwa walio katika mazingira ya huduma za afya, hasa wale wenye magonjwa mengine au kinga dhaifu.
Kwa mtu mwenye afya ambaye hayuko katika mazingira hayo, hatari si sawa na ile ya mgonjwa aliyelazwa hospitalini.
Hata hivyo, kuongezeka kwa C. auris kunasisitiza umuhimu wa hospitali kuwa na mifumo madhubuti ya kugundua, kutenga na kudhibiti maambukizi.
Facts Check:
Candida auris ni fangasi ambao wameibua wasiwasi mkubwa duniani kutokana na uwezo wake wa kuenea katika mazingira ya huduma za afya, kubaki kwenye nyuso na vifaa, pamoja na baadhi ya aina zake kuwa sugu kwa dawa kadhaa za antifungal.
Jambo muhimu ni kutofautisha kubeba fangasi bila dalili na kuwa na maambukizi halisi. Kwa wagonjwa walio katika mazingira ya hospitali, utambuzi wa mapema, usafi wa mikono, usafishaji wa mazingira na udhibiti madhubuti wa maambukizi ni muhimu katika kupunguza kuenea kwa fangasi huyu.
Vyanzo: CNN, US Centers for Disease Control and Prevention (CDC), Johns Hopkins University na Yale University.
